Hadithi za kale zenye mafundisho za Esopo zilizoandikwa zaidi ya miaka 3000 iliyopita. Zimetafsiriwa kwa Kiswahili na Issa S. Kanguni, chini ya shirika lisilo la kiserikali la Tanzania Inventors and Techno-Thinkers Consortium (TITC). Tel; +255757242960

Tafuta katika Blogu Hii

Pages

Jumatatu, 17 Julai 2023

HADITHI YA PETER RABBIT

Pata kitabupepe cha hadithi hii ya mtunzi Beatrix Potter iliyotafsiriwa, kwa bei Tsh. 4,000 tu.
Download Hadithi ya Peter Rabbit
Share:

Alhamisi, 1 Machi 2018

Mbweha na Beberu



Siku moja Mbweha alitumbukia kisimani kwa bahati mbaya, na ingawa kisima chenyewe hakikuwa na kina kirefu sana, alijikuta akishindwa kutoka nje tena. Baada ya kuhangaika kwa muda mrefu bila mafanikio, hatimaye akatokea Beberu mwenye kiu kali. Beberu alidhani kuwa Mbweha ametumbukia kwenda kunywa maji kukidhi kiu yake, na hivyo akauliza kama maji yalikuwa safi au la.

“Ni safi na matamu kupita maji yote kwenye nchi hii,” alijibu Mbweha yule mjanja, “jirushe utumbukie ujionee mwenyewe. Maji ni mengi yanatutosha sote na tutasaza.”

Beberu mwenye kiu mara moja alijitosa kisimani na kuanza kuyafakami maji. Mbweha naye kwa haraka sana alimdandia Beberu mgongoni akachupa kwenye ncha za pembe za Beberu na kutoka zake nje ya kisima.
Yule Beberu mpumbavu akang’amua kuwa amejiingiza matatizoni, akaanza kumbembeleza Mbweha amsaidie kumtoa kisimani. Lakini Mbweha tayari alikwishaanza kutokomea zake mitini.

“Laiti ungalikuwa na akili kama ulivyo na ndevu, rafiki,” alimwambia huku akikimbia zake, “ungalikuwa makini na kujaribu kung’amua kwanza njia utakayoitumia kutokea kisimani kabla hujatumbukia.”

Mwisho.
Share:

Jumatano, 28 Februari 2018

Kisa cha Beberu Wawili

    Mbuzi wawili Beberu walikuwa wakirandaranda kwenye pande mbili za mlima kila mmoja kivyake. Kwa bahati mbaya walikutana kwenye eneo lenye korongo lenye kina kirefu sana ambalo chini yake kulikuwa na mto mkubwa uliotiririka kwa kasi.
    Tawi la mti ulioanguka lilikatiza juu ya korongo hilo na ndo lilikuwa njia pekee ya kuweza kuvuka, na juu ya tawi hilo hata panya buku wawili wasingaliweza kupita kwa pamoja salama. Kwa jinsi njia hiyo ilivyokuwa nyembamba kulinganisha na ukubwa wa korongo, hata kiumbe jasiri vipi angalitetemeka kwa woga.
    Lakini si kwa Beberu wale. Kwa tabia yao ya kiburi na kupenda kujikweza, hakuna mmoja kati yao aliyekuwa tayari kumpisha mwenzie avuke kwanza.
    Basi ikawa, Beberu mmoja alikita miguu kibabe kwenye gogo. Na mwingine naye akafanya vivyo hivyo. Katikati waliinamisha vichwa wakaumanisha pembe zao. Hivyo walianza kusukumana na hatimaye wote walianguka korongoni wakasombwa na maji na kuangamia.

Mwisho
Share:

Jumamosi, 28 Februari 2015

KISA CHA TAUSI NA KORONGO

Tausi, kwa maringo na madaha aliupepeza mkia wake mpana na kumdhihaki Korongo ambaye alikuwa akipita karibu yake, akimtazama kwa dharau kwa kuona rangi ya manyoya yake iliyofubaa na isiyovutia, akamwambia, 
“Ona mimi nimevikwa joho la kupendeza, kama mfalme vile, kwa rangi ya dhahabu na hudhurungi na rangi nyingine zote za upinde wa mvua; ilhali wewe huna hata punje ya rangi ya kuvutia kwenye mbawa zako.”
Tausi akimtambia Korongo

“Ni kweli,” alijibu Korongo; “lakini mwenzio ninaruka na kupaa kwa raha juu angani huku nikipaza sauti yangu kuelekea anga za mbali kwenye nyota, wakati wewe unanatembea chini tu, kama jogoo, miongoni mwa ndege wala vinyesi.”


FUNDISHO; MANYOYA MAZURI HAYAFANYI NDEGE MZURI.
Share:

Jumatatu, 16 Juni 2014

KISA CHA NYANI WACHEZA SHOO

Mwanamfalme aliagiza Nyani kadhaa wapewe mafunzo maalum ya kucheza shoo. Kwa  vile kwa asili Nyani ni waigaji wazuri sana wa matendo ya binadamu, walionyesha kuwa wanafunzi bora wenye kushika mafuzo haraka, na walipovishwa nguo na vinyago kichwani, walicheza vizuri sana hadi kulingana au kwazidi wacheza shoo binadamu. 

Kwenye matamasha maonyesho yao mara nyingi yalishangiliwa kwa vifijo na nderemo, hadi siku moja jamaa fulani mcheza shoo mwenye wivu, aliyepania kuwafanyia hila, alitoa mfukoni mwake karanga za maganda na kuzirusha jukwaani. 
Basi ikawa wale Nyani, baada ya kuona karanga wakasahau kazi yao ya kucheza na wakawa (na kweli walikuwa) Nyani badala ya Wachezashoo
Walivua vinyago vyao na kuchanachana nguo walizovikwa, wakagombania karanga. Hivyo onyesho hilo likaishia hapo huku hadhira ikicheka na kudhihaki.
***
Share:

Kisa cha Wavulana na Vyura


Watoto wavulana, wakiwa wanacheza kandokando ya bwawa, waliona Vyura kwenye maji wakaanza kuwarushia mawe huku wakifurahia mchezo wa kulenga shabaha. 
Waliwaua vyura kadhaa, hadi Chura mmoja jasiri, alipotokeza kichwa chake nje ya maji, na kuwaambia kwa uchungu: 
"Acheni, acheni, enyi vijana: huu ambao ni mchezo kwenu, kwetu sisi ni kifo."
Share:

Kisa cha Mbwa na Mbweha

Mbwa, katika pitapita zao waliikuta ngozi ya Simba, wakaanza kuing'ata na kuirarua vipande vipande kwa meno yao. 

Mbweha aliwaona, akawaambia, 
"Laiti kama Simba huyo angekuwa hai, basi bila shaka mngetambua ya kuwa makucha yake yana nguvu kuliko hata meno yenu."
Share:

Live Traffic Feed

Blogroll

BTemplates.com

Inaendeshwa na Blogger.

Jumla ya Mara Iliyotazamwa

Popular Posts

Kumbukumbu la Blogu